ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

ZIMA KILA KITU ILA WASHA JEMBE FM 93.7 MWANZA

Wednesday, January 28, 2026

DEPU AFUNGA MAWILI YANGA YAICHAPA DODOMA JIJI FC 3-1 MWENGE

 


MABINGWA watetezi, Young Africans, maarufu tu kama Yanga SC wametoka nyuma na kushinda mabao 3-1 dhidi ya Dodoma Jiji FC katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara uliochezwa jana usiku katika  Uwanja wa KMC Complex, Mwenge, Dar es Salaam.

Mabao Yanga SC yamefungwa na washambuliaji wake wa kigeni, Muangola Laurindo Dilson Maria Aurélio ‘Depu’ mawili kwa penalti dakika ya 45’+2 na la kichwa dakika ya 60 na Mzimbabwe, Prince Dube Mpumelelo dakika ya baada ya 66, na hiyo ilikuwa baada ya mshambuliaji mzawa, William Edgar kuanza kuifungia Dodoma Jiji FC dakika ya 41 akiwatoka kwa ustadi mkubwa mabeki wa Yanga kabla ya kumtungua kipa namba moja wa Mali, Djigui Diarra.


Kwa ushindi huo, Yanga SC wanafikisha pointi 22 katika mchezo  wa nane na kurejea kileleni ikiishushia nafasi ya pili JKT Tanzania yenye pointi 21 za mechi 12.


Kwa upande wao Dodoma Jiji baada ya kupoteza mchezo huo wanabaki na pointi 10 za mechi 10 nafasi ya 11.


Baada ya mchezo huo Yanga wanakwenda Zanzibar kujiandaa na mchezo wa marudiano wa Kundi B Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Al Ahly ya Misri Jumamosi ya Januari 31 Uwanja wa New Amaan Complex.


Ikumbukwe Yanga ilichapwa 2-0 na wenyeji, Al Ahly Ijumaa ya Januari 23 mabao ya winga wa kushoto, Mahmoud Ahmed Ibrahim Hassan ‘Trézéguet’ moja kila kipindi, dakika ya 45’+3 na 75 Ijumaa usiku huu Uwanja wa Borg El Arab Jijini Alexandria, Misri.


Saturday, January 24, 2026

YANGA SC YATELEZA UGENINI, YACHAPWA 2-0 NA AHLY ALEXANDRIA

 


TIMU ya Yanga imeteleza ugenini baada ya kuchapwa mabao 2-0 na wenyeji, Al Ahly katika mchezo wa Kundi B Ligi ya Mabingwa Afrika usiku huu Uwanja wa Borg El Arab Jijini Alexandria, Misri. 

Mabao yaliyoizamisha Yanga SC jana yote yamefungwa na winga wa kushoto, Mahmoud Ahmed Ibrahim Hassan ‘Trézéguet’ moja kila kipindi, dakika ya 45’+3 na 75.

Kwa ushindi huo, Al Ahly inafikisha pointi saba kufuatia ushindi wa 4-1 dhidi ya JS Kabylie ya Algeria nyumbani na sare ya 1-1 ugenini dhidi ya wenyeji, AS FAR Rabat nchini Morocco.

Yanga wanabaki na pointi zao nne walizovuna kwenye mechi mbili za awali wakishinda 1-0 nyumbani dhidi ya FAR Rabat na sare ya bila mabao, 0-0 ugenini na JS Kabylie.

Mchezo mwingine wa Kundi B leo, JS Kabylie watawakaribisha AS FAR Rabat Uwanja wa Hocine Aït Ahmed mjini Tizi Ouzou.

Yanga wanarejea nyumbani kuwasubiri Al Ahly kwa mchezo wa marudiano Januari 31 Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar.

𝗦𝗘𝗥𝗜𝗞𝗔𝗟𝗜 𝗬𝗔𝗢𝗠𝗕𝗪𝗔 𝗞𝗨𝗣𝗨𝗡𝗚𝗨𝗭𝗔 𝗭𝗔𝗜𝗗𝗜 𝗚𝗛𝗔𝗥𝗔𝗠𝗔 𝗭𝗔 𝗨𝗦𝗔𝗝𝗜𝗟𝗜 𝗪𝗔 𝗢𝗡𝗟𝗜𝗡𝗘 𝗠𝗘𝗗𝗜𝗔.

Mwenyekiti wa MISATAN na MPC, Edwin Soko (kulia) akimkabidhi Mkurugenzi wa BMG Media, George Binagi, tuzo maalum kutoka YouTube baada ya BMG Media kufikisha zaidi ya wafuasi (subscribers) laki moja.

Serikali imeombwa kuendelea kupunguza gharama za usajili wa vyombo vya habari mtandaoni (Online Media) ili kuongeza fursa za ajira na kujiajiri kwa vijana nchini.

.
Ombi hilo limetolewa Jumamosi Januari 24, 2026 na Mkurugenzi wa BMG Media, George Binagi, wakati wa hafla fupi ya kupokea tuzo maalum kutoka YouTube baada ya BMG Media kufikisha zaidi ya wafuasi (subscribers) laki moja.
.
Akizungumza katika hafla hiyo, Binagi amesema licha ya Serikali kupunguza gharama za usajili wa Online Media kutoka shilingi milioni moja hadi shilingi laki tano, bado kiwango hicho ni kikubwa kwa vijana wengi, hususan wahitimu wa taaluma ya uandishi wa habari na wabunifu wa maudhui, hivyo ameomba gharama hizo zishushwe hadi shilingi laki moja.
 

Ameeleza kuwa hatua hiyo itachochea vijana wengi zaidi kuanzisha vyombo vya habari mtandaoni na kujiajiri, jambo litakalosaidia kupunguza tatizo la ukosefu wa ajira nchini.
.
Aidha, Binagi amesema kuanzia mwaka 2026, watengeneza maudhui mtandaoni wameanza kukatwa asilimia tano ya mapato yao na kuwasilishwa serikalini, huku wakiendelea kulipa kodi nyingine mbalimbali, hali ambayo imewaongezea mzigo wa kodi na kusababisha kile alichokitaja kama kulipa kodi mara mbili.
.
 Kutokana na hilo, ameomba Serikali kulitafutia ufumbuzi suala hilo.
.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa MISATAN na MPC, Edwin Soko, amesema mitandao ya kijamii imeendelea kuwa fursa muhimu kwa vijana katika kukabiliana na changamoto ya ukosefu wa ajira, hivyo amewahimiza vijana kutumia mitandao hiyo kwa njia sahihi na yenye tija.
.
Kuhusu gharama za usajili na masuala ya kodi, Soko amesema atayawasilisha kwa mamlaka husika kupitia vikao mbalimbali vya wadau wa habari ambavyo vinaendelea kufanyika kwa lengo la kuboresha na kukuza sekta ya habari nchini.
.
#YouTube 
#mwanza 
#Habari 
CC: @bmgonlinetv 

Wednesday, January 21, 2026

JKT YATANGAZA NASAFI MAFUNZO YA KUJITOLEA.

news
Mkuu wa Tawi la Utawala wa JKT, Brigedia Jeneral Hassan Mabena

 

JESHI la Kujenga Taifa (JKT) imetangaza nafasi za kujiunga na mafunzo ya kujitolea kwa vijana wa Tanzania Bara na visiwani kwa mwaka 2026 huku likisisitiza nafasi hizo ni bure kwa vijana watakaoomba.

Akizungumza katika Makao Makuu ya JKT, Chamwino Dodoma, Mkuu wa Tawi la Utawala wa JKT, Brigedia Jeneral Hassan Mabena, amesema usahili wa vijana hao utaanza Januari 26 mwaka huu katika mikoa yote ya bara na visiwani.

Amesema utaratibu wa vijana kuomba mafunzo hayo unaratibiwa chini ya ofisi za wakuu wa mikoa na wilaya na vijana wenye elimu ya kuanzia darasa la saba hadi chuo kikuu wanazo sifa za kuomba, akisema watakaochaguliwa wataanza kujiunga katika kambi mbalimbali za JKT kuanzia February 27 hadi Machi nne mwaka huu.

"Mafunzo haya ni bure wazazi au walezi wasikubali kurubuniwa kutoa fedha ili vijana wao wapate nafasi za kujiunga na mafunzo hayo," amesema Brigedia Jenerali Hassan Mabena.

Amezitaja kozi ambazo wanazipa kipaumbele ni zile za taaluma ya Stashahada ya Teknolojia ya Habari, Stashahada ya Mifumo ya Taarifa za Biashara, Stashahada ya Sayansi ya Kompyuta, Stashahada ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT), Stashahada ya Usalama Mtandaoni.

Nyingine ni Shahada ya Sayansi katika Sayansi ya Kompyuta, Shahada ya Sayansi katika Teknolojia ya Habari, Shahada ya Sayansi katika Uhandisi wa Kompyuta, Shahada ya Sayansi katika Teknolojia ya Habari za Biashara,Shahada ya Sayansi katika Usalama wa Mtandao na Forensics ya kidigitali.

"Nitoe wito kwa Watanzania wenye sifa waende kwenye vijiji kata,tarafa zao ili waweze kujiandikisha, nasisitiza  nafasi hizi haziiuzwi ni fursa iliyotolewa bure kwa Watanzania wote," amesema Brigedia Jenerali Mabena 

Mabena amesema Vijana watakaopewa kipaumbele kuchanguliwa ni waliosoma kozi za masulala ya Sayansi pia akawatahadharisha wazazi kuepuka matapeli.

MBOWE: MZEE MTEI HAKUWA NA SHARI NA MTU.

Mbowe: Mtei hakuwa na shari na mtu

Aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Taifa, Freeman Mbowe, amesema Hayati Mzee Edwin Mtei (94), alikuwa ni mtu aliyejenga uhusiano mwema na watu wakati wote.

Mbowe ameeleza hayo Jana Jumanne Januari 20 jijini Arusha, wakati akizungumza na waandishi wa habari alipokuwa msibani.

Akisimulia namna alivyomfahamu Mzee Mtei, Mbowe, amesema hakuwa mtu wa shari, kila alikofanya kazi, alikuwa amejipanga na alikuwa hachagui rafiki ndani na nje ya chama.

Mtei, alifariki dunia usiku wa kuamkia Januari 19 mwaka huu, wakati akikimbizwa kupatiwa matibabu katika Hospitali  ya Selian Jijini Arusha, inayomilikiwa na Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT).

"Hakuwa mtu mwenye njaa, alikuwa ni mtu anayejiweza, akifanya siasa za mageuzi katika mazingira yale...misingi mikuu ambayo mzee huyu ametuachia ni sera. Tulikuwa na waasisi 12 wa CHADEMA." amesema Mbowe.

Mbowe amesema Mtei aliwasaidi kupata uzoefu ndani ya chama husuani masuala ya kifedha.

Amesema alikuwa na ujuzi mkubwa wa masuala ya kodi na sera pamoja na uzoefu mkubwa wa masuala ya kidiplomasia.


Wakati wa uhai wake, Hayati Edwin Mtei aliwahi kuwa Mkurugenzi wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), Kanda ya Afrika, Katibu

Mkuu wa Jumuiya ya Afrika ya Mashariki (EAC), Gavana wa kwanza wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) na Waziri wa Fedha wakati wa uongozi wa Hayati Julius Nyerere.

MWASISI WA SARAFU

Mbowe amesema: "Mzee Mtei, ndiye aliyekuwa mwasisi wa kwanza wa sarafu ya Tanzania, baada ya ile sarafu ya Afrika ya Mashariki baada ya sisi kuanzisha Benki Kuu ya Tanzania (BoT)".

KUUGUA

Mbowe amesema Mzee Mtei ameugua kwa muda mrefu na familia imepokea kwa uzito msiba huo kutokana na rekodi iliyotukuka, aliyoiweka ndani ya chama na Taifa.

Kwa mujibu wa Mbowe, Mzee Mtei alikuwa akipatiwa matibabu katika hospitali mbalimbali, ikiwemo Hospitali ya Nairobi-Kenya, Dar es Salaam na maeneo mengine kadha wa kadha.

Mbowe alisema: "Natambua CHADEMA  wametuma ujumbe katika msiba huu ili kuungana na familia kwa sababu mzee alikuwa ni mwasisi wa chama chetu. Ni kiongozi ambaye bado tulikuwa tunamuheshimu sana katika njia mbalimbali, kwa sababu misingi yote ya CHADEMA huyu ndiye aliyeianzisha"

ASKOFU ROSEMARY AMPONGEZA DKT. BITEKO

 

Na, Ernest Magashi

Askofu wa Kanisa la Ufunuo Jimbo la Geita, Rosemary Mashauri Bendera, amempongeza Mbunge wa Jimbo la Bukombe, Dkt. Doto Biteko, kwa juhudi zake za kuwaletea wananchi maendeleo, huku akiwahimiza wananchi kushirikiana kwa pamoja katika kuijenga na kuendeleza Wilaya ya Bukombe.Pongezi hizo zilitolewa Jumapili ya Tarehe 19 Jan 2026 wakati wa ibada ya shukrani kwa Mungu baada ya kuvuka mwaka 2025 na kuukaribisha mwaka 2026, iliyofanyika katika Kanisa la Ufunuo mjini Ushirombo, wilayani Bukombe.Katika ibada hiyo, Askofu Rosemary aliwaomba waumini kuendelea kuiombea Serikali na viongozi wake ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi. Alitaja baadhi ya miradi ya maendeleo inayoendelea kutekelezwa wilayani humo, ikiwemo ujenzi wa soko la kisasa, stendi ya mabasi na uwanja wa mpira wa miguu, kama vielelezo vya dhamira ya Serikali katika kuboresha maisha ya wananchi.Aidha, Askofu Rosemary aliwatunuku wachungaji 12 daraja la uchungaji kamili na kuwakabidhi vifaa vya kazi, akiwahimiza kumtumikia Mungu kwa uaminifu kwa kushirikiana na Serikali pamoja na jamii zinazowazunguka katika maeneo watakayopangiwa.Vilevile, aliwasisitiza wazazi na walezi kuwekeza katika elimu ya watoto wao kwa kuhakikisha watoto waliofikia umri wa kuandikishwa darasa la awali na kidato cha kwanza wanaandikishwa na kuhudhuria shule, sambamba na jitihada za Serikali za kuendelea kujenga na kuboresha miundombinu ya elimu.Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Bukombe, Dkt. Doto Biteko, katika ziara zake za kikazi hivi karibuni amekuwa akihamasisha wananchi kushiriki kikamilifu katika miradi ya maendeleo kwa kuchangia nguvu kazi, hususan katika ujenzi wa zahanati na shule.Dkt. Biteko amesema Serikali inatarajia kukarabati shule 23 pamoja na miundombinu yake, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuboresha huduma za elimu wilayani Bukombe, huku akisisitiza kuwa jukumu la wazazi na walezi ni kuhakikisha watoto wote wanapelekwa shule kwa wakati.

Monday, January 19, 2026

NI SENEGAL BINGWA AFCON, MOROCCO YALALA NYUMBANI 1-0

 

TIMU ya Senegal ‘Simba wa Teranga’ imefanikiwa kutwaa Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2025 baada ya ushindi wa 1-0 dhidi ya wenyeji, Morocco usiku huu Uwanja wa Prince Moulay Abdellah Jijini Rabat.


Pongezi kwa mfungaji wa bao hilo pekee, kiungo wa ulinzi wa Villarreal ya Hispania, Pape Alassane Gueye dakika ya 94 katika mchezo uliodumu kwa dakika 120.


Hilo linakuwa taji la pili la AFCON kwa Senegal baada ya awali kulibeba mwaka 2021 nchini Cameroon Waliofunga Misri kwa penalti 4-2 baada ya sare ya 0-0 Uwanja wa Olembe Yaoundé.


Nyota wa Senegal, Sadio Mane wa Senegal amechaguliwa Mchezaji Bora wa michuano hiyo (MVP), Mfungaji Bora Brahim Diaz wa Morocco mabao matano, Kipa Bora Yassine Bounou wa Morocco na Timu iliyoonyesha Mchezo wa Kiungwana, Morocco. 

Friday, January 16, 2026

YANGA SC YAACHANA NA KOCHA MSAIDIZI, YAAJIRI MWINGINE NAYE MRENO

 


KLABU ya Yanga imempa mkono wa kwaheri Kocha wake Maaidizi, Filipe Duarte da Silva Pedro baada ya  miezi miwili na ushei tangu awasili na nafasi yake inachukuliwa na Mreno mwingine, Marques Pereira Da Silva.

Filipe Pedro aliwasili Yanga kwa pamoja na Kocha Mkuu, Mreno mwenzake, Pedro Valdemar Soares Gonçalves Oktoba 25 mwaka jana.

Ni uamuzi wa ghafla unaokuja siku chache baada ya Yanga kutwaa Kombe la Mapinduzi wakiiifuga Azam FC kwa penalti 5-4 kufuatia sare ya 0-0 Jumanne Januari 13 Uwanja wa Gombani, Pemba.

Taarifa mbili za Yanga zimeambatana jioni hii — kuondoka kwa Pedro na ujio wa Da Silva ambaye ni Msaidizi wa pili pamoja na Mmalawi, Patrick Mabedi ambaye yupo hata kabla ya ujio wa Kocha Mkuu, Pedro Gonçalves.  
Da Silva

TANZANIA YAVUKA DOLA BILIONI 4 ZA UTALII; YAIPIGA CHINI "DIPLOMASIA YA KIKI" YA MAJIRANI

 

Wakati Kanda ya Afrika Mashariki ikishuhudia ushindani mkali wa kutafuta umaarufu kupitia influencers (washawishi) wa mitandaoni, Tanzania imesisitiza kuwa mafanikio yake katika sekta ya utalii yanatokana na uhalisia na rasilimali zake zisizohitaji 'kupambwa mno' na gharama za serikali.

Kumekuwa na mjadala baada ya ziara ya YouTuber maarufu IShowSpeed nchi jirani,  kuwa ziara hiyo ilikuwa ya kulazimisha ili kupandisha sifa za utalii wa majirani. 

Pamoja na kelele zao za mtandaoni  takwimu za Tanzania zinaonesha kutomhitaji  IshowSpeed katika kutangaza utalii wake.

"Hatuogopi mbinu za kutafuta umaarufu, kwani ukweli wa mazingira yetu, kutoka Zanzibar hadi Serengeti, hauwezi kununuliwa kwa helikopta ya kukodi," alimalizia mchambuzi mmoja wa masuala ya utalii.

Hata hivyo, Rais Samia Suluhu Hassan, katika hotuba yake ya Sherry Party, ametoa jibu la kishindo kupitia takwimu.

 "Tanzania haihitaji kutengeneza hadithi za kufikirika," alisema Rais Samia huku akionyesha kuwa mapato ya utalii yamefikia Dola bilioni 4 mwaka 2025. Huku majirani wakihaha kutafuta umaarufu kupitia TikTok na YouTube, Tanzania imejikita katika kuboresha miundombinu kama SGR na viwanja vya ndege ili kumfanya mtalii wa kawaida awe balozi wa nchi.

Kilimanjaro ni Moja, na Ipo Tanzania 

Ni kama akijibu hoja za baadhi ya nchi jirani kujaribu kujimilikisha alama za Tanzania kama Mlima Kilimanjaro na utamaduni wa Kimaasai, Rais amesisitiza kuwa Dira ya 2050 italinda rasilimali hizo kama mali ya taifa. "Tunajiuza kwa kile tulichonacho. Utulivu wetu na asili yetu ndiyo sumaku kubwa zaidi duniani," aliongeza.

Mkakati wa 'Royal Tour' Unadunda 

Wakati ziara za mastaa wa mtandaoni kama IShowSpeed zikiwa na maisha mafupi (viral for a day), mkakati wa Tanzania kupitia The Royal Tour unaendelea kuleta watalii wa kudumu na wawekezaji wakubwa. 

UCHAGUZI UGANDA 2026: MUSEVENI KINARA WA KURA ZILIZOHESABIWA HADI SASA

 


Uchaguzi Uganda 2026: Museveni achukua uongozi wa mapema wa kura zilizohesabiwa kufikia sasa

Jaji Simon Byabakama, mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Uganda amesema matokeo hayo yanazingatia vituo 133 vya kupiga kura na yanawakilisha asilimia 0.26 ya jumla ya kura zilizopigwa.

Wakati huo huo Rais Museveni amewaonya raia wanaopanga kuandamana siku ya Jumanne akisema kwamba 'wanacheza na moto'.


Mgongano unaokuja  baada ya wimbi la maandamano ya kupingana na serikali yaliyoigonga nchi ya jirani ya Kenya, ambapo watu wasiopunguwa 50 walipoteza maisha katika mapambano na vyombo vya usalama, kulingana na takwimu zilizo chapishwa na Tume ya Kitaifa ya Haki za Binadamu.

Rais Yoweri Museveni, 79, aliyekuwa akitawala taifa la Uganda kwa karibu miongo minne kwa mkono wa chuma, alisema katika hotuba iliyorushwa hewani Jumamosi kuwa maandamano ya kupambana na ufisadi hayataruhusiwa.

“Ana haki gani… unao nayo wa kuleta tabia ya maangamizi? … Tunaanza kuzalisha chakula cha bei rahisi, watu wengine katika sehemu nyingine za dunia wanaachu (kuwa na njaa)… wewe unataka kutulazimisha kuvuruga. Unacheza na moto kwa sababu hatuwezi kukuruhusu kutuvuruga,” Museveni aliweka maneno yake katika hotuba iliyotumia saa tatu.

Wengi wa vijana wa Uganda wanasema kupitia mitandao ya kijamii kuwa wanapanga kuendelea na maandamano hadi ofisi za bunge la taifa, licha ya jeshi la polisi kukataa kutoa vibali vya maandamano.

Jeshi la Polisi wa Uganda liliutanabaisha umma kwa maandamano yaliyopangwa kuwa “yanayoweza kusababisha vurugu” katika taarifa ya Jumatatu, likionya kwamba “hawatahimili tabia ya utulivu mbovu.”

Baadhi ya waandamanaji vijana waliodhamiria kujiunga na maandamano hayo ya Jumanne wameanza kutupia picha zao kwenye mitandao ya kijamii, wakihanikiza  raia wenzao nao wafanye vivyo hivyo ili wapate kuwataja wakirudi salama nyumbani. 

Na hata ikitokea wakapotea basi ijulikane ni kipi kiliwapoteza.



HILI HAPA - BONGE MOJA LA RAGGA LA KUFUNGULIA MWAKA 2026

Thursday, January 15, 2026

YANGA SC YATAMBULISHA STRAIKA MUANGOLA ALIKUWA ANACHEZA ULAYA

 

𝙔𝙖𝙣𝙜𝙖 𝙎𝙘 imemtambulisha mshambuliaji wa Kimataifa wa Angola Lauren do Dilson Maria 'Depu' kuwa mchezaji wake mpya akitokea Radomiak Radom ya Poland.

Je, Depu ana rekodi ya kuthibitisha uwezo wa kufunga mabao?
Depu ana uzoefu mkubwa wa kimataifa akiwa ni mshambuliaji wa timu ya taifa ya Angola, ambapo amefunga mabao mengi kwa nchi yake takwimu zinaonyesha ana takribani 15 mabao katika michezo 18 za kimataifa kwa Angola. 

Pia, katika mashindano ya COSAFA Cup, Depu amekuwa mfungaji bora na mchezaji muhimu sana, akisaidia Angola kushinda mataji na kupata tuzo za Golden Boot. 

Confédération Africaine de Football
Kwa timu za vilabu (club), rekodi yake ya mabao haionekani kuwa ya juu sana katika baadhi ya ligi za Ulaya kama Poland kwa mfano katika Ekstraklasa mwaka wa 2025/26, Depu aliweza kufunga mchezo mmoja kwenye mechi tisa akiwa Radomiak Radom. 

Transfer Feed
Hitimisho: Yanga SC imepata mshambuliaji mwenye uzoefu wa kimataifa na rekodi nzuri ya kufunga mabao kwa timu yake ya taifa, hasa katika mashindano ya COSAFA Cup. Hata hivyo, kiwango chake cha mabao katika vilabu vya Ulaya hakikuwa cha juu sana hivi karibuni hivyo mafanikio yake kama mwarobaini wa uhakika wa mabao kwa Yanga yatategemea jinsi atakavyoweza kuendana na ligi ya Tanzania na uwezo wa benchi la ufundi kulifanya afanikiwe ipasavyo

Tuesday, January 13, 2026

YANGA BINGWA MAPINDUZI CUP 2026

 


FULL TIME MAPINDUZI CUP 

Penalty imeamua matokea Azam Fc 4 - 5 Yanga Sc 

Okelo Mechi 0 Kombe 1

TIMU ya Yanga SC imefanikiwa kutwaa Kombe la Mapinduzi baada ya ushindi wa penalti 5-4 dhidi ya Azam FC kufuatia sare ya bila kufungana ndani ya dakika 120 jioni ya leo Uwanja wa Gombani, Pemba. 


Shujaa wa Yanga SC leo ni mlindamlango, Abdultwalib Mshery aliyeokoa penalti ya beki wa kati raia wa Ivory Coast, Ahoutou Angenor Landry Zouzou.


Waliofunga penalti za Yanga ni washambuliaji Emmanuel Mwanengo, Mzimbabwe Prince Dube, viungo Pacome Zouzoua, Mudathir Yahya na beki na Nahodha, Bakari Nondo Mwamnyeto. 


Waliofunga penalti za Azam FC ni kiungo, Yahya Zayd, beki Twalib Nuru, kiungo raia wa Mali, Sadio Kanoute na mshambuliaji Ngita Kamanya.


Yanga ingeweza kuondoka na ushindi mapema tu kama kiungo wake Muivory Coast, Peodoh Pacome Zouzoua amgefunga penalti dakika ya 115, lakini ikaokolewa na kipa Aishi Salum Manula.


Aidha, Yanga SC pia ilishindwa kutumia mwanya wa Azam FC kucheza pungufu tangu dakika ya 55  baada ya winga wa Kimataifa wa Mali, Cheickna Diakité kutolewa kwa kadi nyekundu kufuatia kuonyeshwa kadi ya pili ya njano. 

ALLAN OKELLO NI MCHEZAJI MPYA WA YANGA SC

 


KLABU ya Yanga  ya nchini Tanzania imemtambulisha rasmi winga wa Kimataifa wa Uganda Allan Okello (21) kuwa mchezaji wake mpya akijiunga na Wana Jangwani hao kutoka Vipers FC ya kwao.

REAL MADRID YAMTIMUA ALONSO BAADA YA KIPIGO CHA BARCA

 

VIGOGO wa soka wa Hispania, Real Madrid wametangaza kwamba meneja wao, Xabi Alonso, ameondoka klabuni kwa makubaliano ya pande zote mbili baada ya michezo 28 pekee.

Kiungo huyo wa zamani wa Liverpool aliteuliwa mwanzoni mwa msimu huu baada ya kuondoka Bayer Leverkusen, ambayo aliiongoza kutwaa ubingwa wa Ujerumani mwaka 2024.

Nafasi yake imechukuliwa na mchezaji mwingine wa zamani wa Liverpool, Alvaro Arbeloa, ambaye amekuwa kocha wa timu B ya Real Madrid tangu Juni mwaka jana na pia alitumia miaka sita iliyopita akifanya kazi na akademi.

Alonso anaondoka Real ikiwa inashika nafasi ya pili kwenye msimamo wa La Liga, ikizidiwa pointi nne na wapinzani wao, Barcelona katikati ya msimu.

Alipata asilimia bora ya ushindi kuliko kocha mkuu yeyote wa Real Madrid katika muongo mmoja uliopita. 

Lakini klabu hiyo ilifungwa mabao 3-2 na vinara wa La Liga, Barcelona, ​​katika mchezo wa Fainali ya Super Cup ya Hispania Jumapili ikiwa ni mwaka wa pili mfululizo wanapoteza.

Kikosi cha Alonso pia kimepoteza kwa Liverpool na Manchester City katika Ligi ya Mabingwa msimu huu. Real ilimaliza ya pili katika LaLiga msimu uliopita.

Real Madrid ilisema klabu hiyo iliachana na Alonso kwa "makubaliano ya pande zote".

"Xabi Alonso atakuwa na mapenzi na pongezi kutoka kwa mashabiki wote wa Madrid kwa sababu yeye ni gwiji wa Real Madrid na amekuwa akiwakilisha maadili ya klabu yetu," taarifa ilisema. "Real Madrid itakuwa nyumbani kwake kila wakati."

Alonso hapo awali alihusishwa na kuhamia Liverpool wakati Jurgen Klopp alipotangaza kwamba angeondoka Anfield mwaka 2024 - lakini akachagua kubaki Leverkusen kwa msimu mwingine kabla ya kuhamia Madrid.

Alisaini mkataba wa miaka mitatu mwezi Mei kumrithi Mtaliano Carlo Ancelotti, ambaye aliondoka klabuni hapo na kuwa kocha mkuu wa Brazil.

Alijijengea heshima kubwa baada ya kuifunga Barcelona 2-1 Uwanja wa Bernabeu Oktoba mwaka jana na kukataa uteja wa kufungwa mechi sita mfululizo na mahasimu wao hao, lakini Real ilishinda mechi mbili tu kati ya nane zilizofuata katika mashindano yote. 

Sunday, January 11, 2026

MASHABIKI WA SIMBA USO KWA USO NA MASHABIKI WA PAMBA JIJI


 Ni Januari 12, 2026… Mwanza inawaka moto wa sherehe!!

Katika kuadhimisha Siku ya Mapinduzi ya Zanzibar, jiji la Mwanza linawaletea burudani ya kipekee, mechi ya kirafiki ya kihistoria… Mashabiki wa Simba vs Pamba Jiji!

Watachuana mastaa wa zamani waliowahi kung’ara kwenye timu hizi mbili maarufu nchini – ni kumbukumbu, ni burudani, ni hadithi za mpira zinazofufuka tena!

Na si mpira tu! Kutakuwa na michezo ya kina dada, kina mama, zawadi kibao na burudani ya nguvu kwa familia nzima!

Jumatatu ya tarehe 12 Januari 2026, kuanzia saa nane mchana, pale Uwanja wa Nyamagana – usikose kushuhudia historia ikiandikwa upya!

MAPINDUZI DAY – Mwanza inasherehekea kwa mshikamano, amani na burudani ya kufungia mwaka!

Mgeni rasmi: Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mh. Said Mtanda

GGML YATOA MSAADA WA MILIONI 50 KUSHEREHEKEA MWAKA MPYA NA WATOTO YATIMA

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Geita Gold Mining Limited (GGML) Bw. Duan Campbell (kati kati) akipeana mikono na Mkuu wa Mkoa wa Geita Mh.Martine Shigela (wa tatu kutoka  kulia) baada ya kukabidhi mfano wa hundi ya shilingi milioni 50 kwa kituo cha Watoto Yatima cha Moyo wa Huruma kilichopo mkoani Geita mwishoni mwa wiki. Kituo hicho kimeanzishwa kwa ushirikiano wa pamoja kati ya GGML , Halmashauri ya Geita na Kanisa Katoliki . Wa pili kwa upande wa kulia ni Askofu  Flavian Kasala wa Jimbo Katoliki la Geita.

 Na Mwandishi Wetu, Geita

Kampuni ya Geita Gold Mining Limited (GGML) imeendelea kuthibitisha dhamira yake ya uwajibikajo kwa jamii kwa kutoa msaada wa hundi ya shilingi milioni 50 kwa kituo cha kulelea watoto yatima cha Moyo wa Huruma wakati wa sherehe za kuukaribisha mwaka mpya 2026 zilizofanyika kituoni hapo, mkoani Geita  mwishoni mwa wiki.


Akizungumza wakati wa hafla ya kukabidhi mfano wa hundi hiyo kwa uongozi wa kituo hicho, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa GGML, Bw. Duan Campbell, amesema uwepo wa GGML katika moa wa Geita haujikiti tu katika uchimbaji wa dhahabu bali pia katika kuigusa jamii kwa kujenga jamii yenye afya, matumaini na fursa hasa kwa Watoto walioko katika mazingira magumu.


“Kujenga jamii yenye afya na yenye matumaini ni sehemu ya jukumu letu kama kampuni inayojishughulisha na uchimbaji wa madini. Uwekezaji wetu katika maendeleo ya kijamii unaendelea kuwa kichocheo cha ukuaji wa ndani, kikanda na kitaifa. Tunajivunia kushirikiana na Moyo wa Huruma na kuona jinsi maisha ya Watoto yanavyobadilika kwa misaada na fursa wanazopata.


“Tunajisikia fahari kuona watoto wanaolelewa katika kituo hiki wanapata mafanikio, ikiwemo wale wanaohitimu katika vyuo vikuu,”


“Hivyo, kama wadau wa maendeleo ya jamii, GGML tutaendelea kuhakikisha kuwa kituo hiki kinapata mafanikio zaidi na kushirikiana na Serikali katika kutokomeza watoto wa mitaani,” amesema Bw. Campbell. 


Kituo cha Moyo wa Huruma kilianzishwa mwaka 2006 kupitia ushirikiano kati ya GGML, Jimbo Katoliki la Geita na Halmashauri za Serikali ya mkoa wa Geita, kama sehemu ya mkakati wa muda mrefu wa kukabiliana na changamoto za watoto yatima na wanaoishi katika mazingira magumu—ikiwemo watoto waliopoteza wazazi kutokana na VVU/UKIMWI.


Kupitia mfuko wa GGML Kili Challenge Against HIV & AIDS, GGML imekuwa ikishirkiana na wadau mbalimbali ikiwemo Tume ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania (TACAIDS) kukusanya rasilimali kwa kupanda Mlima Kilimanjaro kwa lengo la kusaidia watu wanaoishi na VVU pamoja na taasisi zinazohudumia makundi yaliyo katika hatari, ikiwemo Kituo cha Moyo wa Huruma. Juhudi hizi zimewezesha kujengwa kwa kituo hicho ambacho kimeweza kukua kutoka kulea watoto 12 mwaka 2006 hadi kuwahudumia zaidi ya watoto 100 kwa sasa, wakiwemo wahitimu wa vyuo vikuu na watumishi wa umma.


Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mh. Martine Shigela ambaye alikuwa mgeni rasmi katika hafla hiyo, ameipongeza GGML kwa kuendelea kusaidia makundi mbalimbali katika jamii.


“Napenda kuwapongeza GGML kwa ibada hii ya kulea kituo hiki chenye watoto wakiwemo watoto wadogo na wakubwa ambao baadhi yao ni wahitimu wa vyuo vikuu mbalimbali wanaosomea masomo ya Sayansi na wale walioajiriwa Serikalini ambao wamepitia katika kituo hiki,” amesema RC Shigela


Akizungumza katika hafla hiyo, Askofu wa Jimbo Katoliki la Geita, Askofu Flavian Kasala amesisitiza umuhimu wa jamii kuendelea kushirikiana katika kujiepusha na kuzuia vyanzo vinavyopelekea ongezeko la watoto wanaoishi katika mazingira magumu ambao hukosa msaada na hatimaye kutapakaa mitaani.


“Matatizo mbalimbali katika jamii ikiwemo changamoto zinazotokana na uzazi katika umri mdogo, maambukizi ya Virusi vya UKIMWI na ugumu wa maisha yamepeleka uwepo wa watoto wa mitaani wenye uhitaji kutoka katika jamii”


“Hivyo, kituo kama hiki, kinatupa somo la kuwapa faraja watoto wenye uhitaji na kuweka jitihada za makusudi za kuzuia ongezeko la watoto hao wanaoishi katika mazingira magumu,” amesema Askofu Kasala.


Akizungumza mara baada ya hafla ya kukabidhi hundi, Mwakilishi wa GGML kutoka idara mahusiano Mussa Shunashu ameeleza majukumu ya GGML katika kituo hicho kilichoanzishwa kwa ushirikiano kati ya GGML, Jimbo Katoliki la  Geita na Halmashauri za Mkoa wa Geita.


“GGML katika kuanzisha na kuendeleza kituo hiki, ilikuwa na wajibu wa kutoa fedha na halmashauri wakati huo ilikuwa na wajibu wa kutoa eneo na Jimbo Katoliki la Geita lilikuwa na wajibu wa kusimamia malezi bora na tunashukuru mpaka leo hii kituo hiki kinaendelea kutoa huduma,” 


“Kama ilivyo katika mikoa mingine, mkoa wa Geita pia una watoto yatima, ambao walipoteza wazazi/ walezi kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo ugonjwa wa UKIMWI, hivyo, tuliamua kuwa na kituo hiki kwa msaada wa malezi na elimu kwa watoto wenye uhitaji,” amesema.


Katika hafla hiyo ya kuadhimisha Mwaka Mpya 2026, GGML pia ilitoa zawadi mbalimbali, kuandaa burudani, michezo na chakula kwa watoto na walezi wao, pamoja na mazungumzo ya faraja yaliyoimarisha dhana ya malezi ya pamoja na mshikamano wa kijamii.


Mmoja wa watoto wanaolelewa katika kituo hicho (jina limehifadhiwa) amesema msaada unaotolewa na GGML na wadau wengine umewapa nguvu ya kuota ndoto kubwa.


“Tunajisikia kama tupo nyumbani. Tunathamini sana kuona kuna watu wanaojali maisha yetu na mustakabali wetu,” amesema mtoto huyo.


Hatua hii inaendelea kuonesha utekelezaji wa sera ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR) ya GGML, inayolenga kuimarisha afya, elimu na ustawi wa watoto na familia katika mkoa wa Geita na Tanzania kwa ujumla, kwa kutambua kuwa maendeleo endelevu huanza na uwekezaji kwa watu.

MADAKTARI IRAN WADAI KUZIDIWA NA WAGONJWA

 


Huku maandamano nchini Iran yakiendelea na mamlaka ya Iran ikitoa maonyo yaliyoratibiwa kwa waandamanaji, daktari na muuguzi katika hospitali mbili waliiambia BBC kwamba vituo vyao vya matibabu vilikuwa vimejaa watu waliojeruhiwa.

Daktari mmoja alisema hospitali ya macho ya Tehran ilikuwa iko katika hali ngumu, huku BBC pia ikipokea ujumbe kutoka kwa daktari katika hospitali nyingine ikisema haikuwa na madaktari bingwa wa kutosha kukabiliana na ongezeko la wagonjwa.

Siku ya Ijumaa, Rais wa Marekani Donald Trump alisema Iran ilikuwa katika "matatizo makubwa" na akaonya "ni vyema isianze kufyatua risasi kwa sababu sisi pia tutaanza kufyatua risasi".

Katika barua kwa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, Iran iliilaumu Marekani kwa kuyageuza maandamano hayo kuwa kile ilichokiita "vitendo vya uasi na uharibifu mkubwa".

CHANZO BBC SWAHILI

MISRI YAWAVUA UBINGWA IVORY COAST NA KUTINGA NUSU FAINALI AFCON

 

TIMU ya Misri imefanikiwa kwenda Nusu Fainali Kombe la Mataifa ya Afrika baada ya ushindi wa mabao 3-2 dhidi ya mabingwa watetezi, Ivory Coast usiku wa jana Uwanja wa Adrar mjini Agadir nchini Morocco. 

Mabao ya Mafarao jana yamefungwa na mshambuliaji, Omar Khaled Mohamed Abdelsalam Marmoush wa Manchester City dakika ya nne, beki Ramy Hisham Abdel Aziz Mostafa Rabia wa Al Ain ya Falme za Kiarabu (UAE) dakika ya 32 na kiungo mshambuliaji, Mohamed Salah anayekiputa Liverpool dakika ya 52.

Kwa upande wao mabingwa wa Fainali za 2023 nyumbani, Ivory Coast mabao yao yalifungwa na beki wa kushoto wa Zamalek,  Ahmed Mohamed Abou El Fotouh Mohamed aliyejifunga dakika ya 40 na beki wa kulia wa Strasbourg ya Ufaransa alikozaliwa dakika ya 73.

Kwa matokeo hayo, Misri itakutana na Senegal katika Nusu Fainali Jumatano ya Januari 14 kuanzia Saa 1:00 usiku Uwanja wa Tangier Grand mjini Tangier, wakati Nusu Fainali nyingine wenyeji, Morocco watamenyana na Nigeria siku hiyo hiyo kuanzia Saa 4:00 usiku Uwanja wa Prince Moulay Abdellah Jijini Rabat.

NIGERIA YAICHAPA ALGERIA 2-0 NA KUTINGA NUSU FAINALI AFCON

 

TIMU ya Nigeria imefanikiwa kwenda Nusu Fainali Kombe la Mataifa ya Afrika baada ya ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Algeria usiku huu Uwanja wa Marrakech Jijini Marrakech nchini Morocco.

Nigeria ilipata ushindi wa 2-0 dhidi ya Algeria katika robofainali ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2025 Uwanja wa Marrakech Jumamosi, na kujikatia tiketi ya kutinga nusu fainali dhidi ya wenyeji Morocco Jumatano saa 9 alasiri. (saa za ndani) katika Uwanja wa Rabat wa Prince Moulay Abdellah.

Victor Osimhen alitangulia kufunga katika dakika ya 47, akitumia vyema mpira wa Alex Iwobi. Mshambulizi huyo aliipita ngome ya Algeria kabla ya kumtungua kipa Alexandre Zidane na kuwapa Super Eagles bao la kuongoza mapema kipindi cha pili.

Dakika kumi tu baadaye, Akor Adams alifunga bao la Nigeria mara mbili katika dakika ya 57. Osimhen tena alichukua jukumu muhimu, kutengeneza nafasi na kutoa pasi nzuri kwa Adams, ambaye alimaliza kwa utulivu mbele ya Zidane na kufanya matokeo ya mwisho kuwa 2-0.

Algeria, inayojulikana kwa safu duni ya ulinzi katika michuano hiyo, imefungwa kwa mara ya kwanza kwenye mechi hii.